Saturday, March 19, 2016

INAKUPASA KUENENDA KAMA YESU ALIVYOENENDA

Posted by Savior Ministry at 2:50 AM 1 Comment


Kama Yesu Mwenyewe katika siku za Mwili Wake alijifunza kumtolea Yeye awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu, mimi na wewe ni nani hasa tusiwe tunamtolea Mungu maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi?

Kama Yesu uchaji Wake ulipimwa kwa sababu ya vile alivyokuwa anamshirikisha Mungu changamoto Zake kwa kuomba na dua pamoja na kulia sana na machozi, mimi na wewe uchaji wetu unapimwaje?

Kama Yesu alijifunza kutii kwa mateso yaliyompata, hivi mimi na wewe tukipatwa na mateso na changamoto huwa tunatii kwa kumtolea Mungu maombi, dua pamoja na kulia sana na machozi au ndo kila tukipatwa na majanga tunatafuta watu watuombee wao, wakeshe kwa ajili yetu wao, wafunge wao?

Mpendwa acha kuendelea kumkosea Mungu na kumtenda Mungu dhambi kwa kutokuomba.

Kesha na kuomba usije ukaingia majaribuni.

Kukesha katika kuomba sio lazima iwe usiku kucha.

Yesu aliwauliza wanafunzi Wake je hamkuweza kukesha nami japo saa moja?

Ninaamini kukesha katika maombi ni kuomba mpaka mzigo wa lile unaloombea ukuachie.

Shida yetu kubwa ni kwamba hatuombi.

Hatunayo majibu ambayo Mungu anatamani kutupa kwa kuwa hatuombi na hata tukiomba hatupati kwa kuwa twaomba vibaya.

Mpendwa njia ya pekee ya kuwa mzuri katika kuomba ni kujinidhamisha kuamka kuomba na sio unakumbatiana na shuka mpaka ndege wakuamshe asubuhi.

Amka kabla ya hao ndege uombe mpendwa wangu.

Kama unadai kuwa unakaa ndani ya Yesu imekupasa kuenenda wewe mwenyewe kama Yeye alivyoenenda (I Yohana 2: 6).

Kumbuka kuwa Yesu alituachia kielelezo tufuate nyayo Zake (I Petro 2: 21) na Yeye alikuwa ni mtu aamkaye mapema ili kuomba.

“Hata alfajiri na mapema sana akaondoka, akatoka akaenda zake mahali pasipokuwa na watu, akaomba huko.” (MK. 1:35 SUV).

Jenga tabia na palilia nidhamu ya kuamka mapema ili uombe.

Barikiwa sana.

Share This Post

Get Updates

Subscribe to our Mailing List. We'll never share your Email address.

1 comment:

The Savior Ministry Live Chat

© 2016 Savior Ministry.
Powered by Themes24x7 .
back to top