Tuesday, May 7, 2013

Raisi Kikwete aagiza vyombo vya usalama kuwasaka waliolipua bomu kanisani

Posted by Savior Ministry at 4:00 AM 0 Comments
mlipuko

Baada ya mlipuko uliotokea kanisa la Katoliki la Mt. Joseph la Olasiti jijini Arusha, Raisi Kikwete ametoa tamko lifuatalo:-

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amepokea kwa mshtuko na masikitiko makubwa taarifa ya tukio la leo, Jumapili, Mei 5, 2013 la mlipuko kwenye Kanisa Katoliki la Mt. Joseph Mfanyakazi la Olasiti Jijini Arusha. Tukio hilo la kigaidi limesababisha mtu mmoja kupoteza maisha na wengine 40 kujeruhiwa. Rais Kikwete analaani vikali shambulio hilo lililofanywa na mtu au watu katili, waovu na wenye dhamira mbaya na nia mbaya kwa Tanzania na watu wake.

Rais Kikwete ameagiza vyombo vya usalama nchini kumsaka mtu au watu waliohusika na kitendo hicho kiovu na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria. Vile vile Rais Kikwete amewataka wananchi wote kuwa watulivu wakati Serikali na vyombo vyake inaendelea kufuatilia tukio hili. Tutawasaka popote walipo na kupambana nao bila huruma. Aidha, tutakabiliana na aina yoyote ya uhalifu nchini iwe ni ugaidi au aina yoyote ya uhalifu wa namna hiyo au wa namna nyingine, uwe na chimbuko lake ndani ya nchi ama nje ya nchi yetu. Kamwe hatutakubali kuwaacha wavuruge amani na usalama wa Tanzania na watu wake. Rais anaamini kuwa Serikali, kwa msaada na ushirikiano wa wananchi, watu hao watapatikana na kuadabishwa ipasavyo.

Aidha, Rais Kikwete anatoa rambirambi za dhati ya moyo wake kwa wafiwa na wale wote ambao wamejeruhiwa katika tukio hilo. Anaungana nao katika machungu na msiba. Rais pia anawaombea wote walioumia katika tukio hili wapate nafuu ya haraka na waendelee na shughuli zao za ujenzi wa taifa.

Rais Kikwete vilevile anatoa pole nyingi kwa viongozi na waumini wa Kanisa Katoliki kwa tukio hili la kusikitisha na kuvurugika kwa ibada na shughuli yao muhimu ya uzinduzi wa Kanisa lao.

Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
IKULU,
DAR ES SALAAM
5 Mei, 2013

——————————————-

Kwa mujibu wa BBC wametangaza jumla ya watu watatu wameuawa kutokana na mlipuko huo.

——————————————-

UPDATE:

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete leo, Jumatatu, Mei 6, 2013, alikatiza ziara yake ya Kiserikali nchini Kuwait ili kurejea nyumbani kutokana na tukio la shambulio la kigaidi la mlipuko mjini Arusha. Viongozi mbali mbali wa kikristo na serikali wameenda hospitali kuwajulia majeruhi wengine kujitolea damu.

Tags:

Share This Post

Get Updates

Subscribe to our Mailing List. We'll never share your Email address.

0 Comments:

The Savior Ministry Live Chat

© 2016 Savior Ministry.
Powered by Themes24x7 .
back to top